Padili James Mikomangwa
Imekuwa desturi kwa wanadamu kunyambua kila jambo
linaloletwa mbele yao, tokea kuanzishwa kwa misingi ya dunia kuchanganua mambo
kwa kina imekua tabia yetu. Tumeona kwa mifano mingi hai kwa watu wanaoweza
kufikiri kwa weledi(ulimwenguni kote)
hujikuta wakifanikiwa katika kila nyanja ya maisha na wale wanaofanya kinyume cha
hapo mara nyingi mwisho wao huwa si mzuri sana kusimulia hata ikiwa kama
hadithi kama ile ya mzee tola.
Si jambo la kubeza wala kuongelea sana kwa vile lulu za
fikra pevu huokoa zaidi kuliko ndimi zinazo nena sana. Je? Jamii zetu ziko
katika uwanja upi wa fikra ?, ni ule wenye fikra pevu zinaweza ongelea mambo
magumu na kuyapatia maelezo makini na si majibu rahisi au ule uwanja wa
wachezaji wengi wasio na ujuzi wa kufikiri?.
Yamkini kufikiri kunaweza kuwa na tafsiriwa tofauti sana
na watu wa haiba kadha wa kadha , ili kuweka mambo sawa tunaweza sema: kufikiri
ni hatua inayochukuliwa na mwanadamu mwenye akili timamu inayohusisha kunyambua
mambo mbalimbali yenye utata na kinzani , pima mantiki katika hoja , angalia
umuhimu wa mambo kwa jicho makini zaidi ya lile la nyama na kupata hitimisho
lililosheheni maamuzi chanya na yakinifu.
Mara nyingi kufikiri kunahitaji muda, utulivu wa nafsi,
mwili na akili yako kwa ujumla. Ni nadra sana kukuta maamuzi chanya yanachukuliwa
pale mtu anapofikiri kwa pupa na akiwa na mihemuko, kwa vile akili zetu
huzidiwa na mihemuko inayochukua sehemu ya ubongo wenye uwezo wa kutambua mambo
kwa weledi.
Jamii zetu zimekuwa na mabadiliko makubwa sana ya
kitamaduni, kiteknolojia, kisiasa na katika Nyanja mbalimbali za kimaisha
zinazopatikana katika nchi za ukanda wa chini ya jangwa la sahara kama Tanzania.
Lakini kabla ya kwenda mbali zaidi, jamii ni nini hasa?.
Tunaweza kusema
jamii ni muunganiko wa watu wanaoishi katika eneo Fulani la kijiografia wenye
tamaduni, mila, desturi, historia, lugha moja inayowaunganisha na mifumo ya
uchumi. Katika taifa linalokua kiuchumi lenye watu zaidi ya million 50, jamii
zake zitakuwa na mchanganyiko wa mambo kadha wa kadha hasa hasa tamaduni , mila
na desturi zinazounda utu wa watu.
Tangia kupata uhuru tumekuwa na mabadiliko chanya katika
ulingo wa maendeleo, ambapo tumeona na tunazidi shuhudia teknolojia ikichukua
hatamu katika kubadili maisha yetu. Wimbi kubwa limekuwa la vijana wanaobadili
namna maisha yanavyoendeshwa, na hi inatokana na uwezo mkubwa wa vijana wa
karne ya 21 kujihuisha kirahisi na mabadiliko ya teknolojia pevu duniani
inayochegeza ubadilishwaji wa maisha yetu ya kale na yaliyopitwa na wakati
(yakiwa maoni ya wakosoaji baadhi) na kuangalia maisha mapya ya dunia kiganjani
na utumiaji wa mitambo imara kufanya kazi ambazo zilifanya na binadamu
kupunguza nguvu kazi ambayo haipati mbadala, yote hayo ni kuokoa muda na
gharama za uzalishaji.
Siwezi elezea kwa maneno mengi juu ya jamii zetu lakini
kwa mtu mwenye nia ya dhati na chachu ya maendeleo ya kweli, atajua kuwa kwa
miongo 3 iliyopita kumekuwa na tofauti kubwa sana kwa watu hasa hasa pale
wanapotakiwa kunyambua mambo nyeti , rahisi, yenye kuzua hisia na hata pumba
kwa weledi.
Tumekuwa tukiona mihemuko ikichukua hatamu pale porojo
za siasa zinapoingia na kuchukuliwa kama mantiki, kelele zisizo na msingi
kuandikwa kama hoja na watu tuliowaamini kutupa habari za kina kila kukicha,
tunashuhudia pale hoja za uchumi, elimu na habari za kutatanisha zinapo ibua mijadala
isiyoleta suluhisho endelevu. Haya yote yanatokea mbele ya macho yetu na ni
matokeo ya jamii kulaza akili na kuwaachia watu wachache wasio na ujuzi wa
kunyambua hoja nyeti jukumu la kufikiri kwa niaba yetu.
Wakati nakua sikuwahi kuona wana jamii wenzangu waki
payuka maneno yasio na msingi juu ya hoja waliyosikia tena kupitia mtu baki au
chanzo chochote cha habari ukilinganisha na sasa, nakumbuka walisisimuka kama
wengine (ni asili ya binadamu pale mambo yanayotuhusu yakihusika) lakini
walikaa wakatuliza vichwa na kuanika hoja mezani kujaribu kudadavua kabla ya
kuhukumu.
Mtiririko huu ni
muhimu sana kwa mtu yeyote kuufuata maana utaokoa nguvu, maumivu na majuto
mengi (sote tunajua hasara ya kinyume na hili) lakini kwa karne hii yenye
utandawazi, teknohama makini na ujuzi wa habari kwa haraka sana inashindwa
tekeleza kazi hii ndogo. Inashangaza sana
na mbaya zaidi kuto kuhimili misingi hii ya fikra kunagharimu sana
kushinda tunavyoweza fikiri. Ikumbukwe kuwa si kila msomi au mtu mwenye ujuzi
wa mambo mengi anaweza kuwa na weledi wakufikiri kwa kina, kwa sababu kufikiri
kwa kina kunahitaji utulivu na uwezo wa kuweka mambo bayana, na kuona vitu
katika pande zote jambo ambalo si kila mtu anaweza fanya kirahisi, hata kama ni
mhitimu wa elimu ya juu.
Wana jamii wanapoweza kujenga misingi na tamaduni ya kufikiri
kwa kina ni vigumu sana kwa hoja za kijuha, pumba, uzushi na kelele za watu
walio shika hatamu katika ngazi mbali mbali kwenye jamii kusambaza hoja zao
zisizo na mashiko zilizo undwa kusambaratisha umoja wetu na mshikamano
tuliojenga kwa nguvu kubwa. Jamii zetu zinaundwa na watu wa rika mbali mbali,
wenye tofauti za kichumi, elimu, maoni
ya kisiasa, imani na tamaduni. Kitu cha kujivunia juu ya Tanzania yetu ni
kwamba tumekuwa tukiheshimu tofauti hizi baina yetu kwa muda mrefu sasa,
lakini tokea mitandao ya kijamii
ilipochukua nafasi ya kujamiana iliyokuwepo kabla, tumedhihirisha kabisa kuwa
teknolojia inabadili namna akili zetu zinavyofikiri hasa kwa sasa ambapo kuna wimbi kubwa la hoja tata
zinazojadiliwa na watu wasio na weledi wa kufikiri kwa kina ambao tunawapa
jukumu kubwa kama ‘’ wachambuzi wa mambo mtambuka yanayohusu Tanzania hasa
siasa’’.
Hakuna jambo lolote ambalo linaweza katiza mbele yetu
lisilo na mashiko kwetu na kwa kizazi kitakachofuata likakubalika kirahisi
endapo tuta ichukua misingi ya fikra pevu na kuithamini kama tunavyojithamini
sisi na simu zetu za mkononi. Hatari ya kutofikiri kwa kina kama jamii hujongea
pale mambo muhimu sana yanapo jadiliwa kwa namna rahisi, isiyo jenga na
kupelekea kufanya kwa maamuzi yasiyokuwa endelevu kwa manufaa ya jamii na
kizazi kijacho.
Tuna shuhudia sasa namna masuala ya huduma za kijamii
kama vile afya na elimu kwa kuanzia yanawekwa kando na mkumbo wa siasa ukichukua
hatamu. Hata kama tukiyajadili hatu fanikiwi kupata upembuzi yakinifu na kupata
mipango yakinifu na hata ile sehemu kubwa ya watu wenye ushawishi na
wanaotegemewa kubadili akili za watu ( na inashangaza kwa jamii yetu kuwapa
vinara wa mitandao ya kijamii nafasi nyeti sana) ndani ya jamii haifainikiwi
kutatua mambo haya.
Sio kwamba hakuna kabisa watu wenye uwezo wa kufikiri
kwa kina, watu hawa wapo ndani ya familia zetu huenda wakawa ni wenzi, wazazi,
watoto , kaka hata dada ambao hawasikilizwi kwa kina kama vinara wa migomo
mavyuoni na waandishi wa taarifa zisizo na mashiko mitandaoni kila kukicha.
Kwa muda sasa kama taifa tumeacha kusoma vitabu na maandiko mbalimbali
kujijazia maarifa kwa muda mrefu licha ya kwamba teknolojia ina rahisisha
upatikanaji wa taarifa lakini hatuna taarifa za muhimu. Nashindwa kuelewa ni
wapi tulipojisahau ambapo tukaziacha njia kuu zenye kutupeleka katika maarifa
yanayotuongoza katika maisha, yamkini mabadiliko ya maisha ya mwanadamu au hali
ya kiuchumi, hali ya yote ulinzi wa vichwa vyetu ni muhimu sana kuliko kitu
chocote maana akili inayofikiri japo kidogo haiwezi tekwa na maneno ya watu
yasiyo na umuhimu.
Naona ni muhimu sana kuanza wajenga vijana wetu na
watoto jinsi ya kufikiri na kujua kuchambua kati ya mantiki na upuuzi, kauli
tata na kauli za kijuha, ukweli na uongo, pamoja na hadithi za kila siku zinazo andikwa
na watu mashuhuri wasio na ujuzi wa kufikiri. Kwa sasa tunapokea mambo mengi
sana yanayoingia toka nchi za nje ya bara la Afrika na Tanzania kwa ujumla ,kwa
hiyo si jambo rahisi na ikumbukwe kuna vita vya kiuchumi na kielimu ambavyo
vinatekelezwa kwa weledi mkubwa sana (wengi wetu hatujui) na kama jamii zetu
ziko gizani tutegemee majanga makubwa sana yatakayo tugharimu utu wetu na uhuru
wa kufikiri kwa vizazi na vizazi.
Ni hatari sana kwa jamii, pale inapojulikana kuwa haina
uwezo mkubwa wa kuchambua mambo, kwa sababu yeyote mwenye uwezo wa kukamata
hisia na akili za watu anaweza penyeza lolote kwa jamii na kuivuruga vuruga
kabisa. Haya yanaonekana wakati wa shughuli za kisiasa, shughuli za kiimani,
sherehe na mikumbo isiyokuwa endelevu ni
ishara ya jinsi watu wetu wanavyofuata hisia za watu wachache wenye ushawishi. Dunia
tunayoishi haina huruma kwa roho isiyo na akili inayoweza pembua hoja,
tutaburuzwa na wanaojua kufikiri mpaka kiama, kama tukianza jiimarisha katika
nyaja hii tutakuwa hatari na hakuna wa kutubabahisha kamwe.
Kwa sasa ni nadra sana kwa wale wenye elimu na nafasi ya
kusema kupitia mitandao ya kijamii, kuwaona wakitetea haki za wanyonge na wasio
na uwezo wa kufikisha vilio vyao. Ni watu wachache sana (pongezi kwao)
wanaotekeleza jukumu hili, bahati mbaya hawapati nafasi ya kupanuka kwa sababu
maisha ya watu mashuhuri ni muhimu sana kuliko kuzijua takwimu za kiuchumi, kujadili
soka ni lulu kwetu kuliko kutatua adha za maji kama wanajamii na si mashabiki
wa siasa.
Vita vya dhidi ya akili zetu na uhuru wa kufikiri vipo
hai na vinazidi pamba moto, wengi wetu hatujui kama vita hivi ni kweli au la,
lakini nipende kukuhakikishia kuwa ni
vita hatari kushinda tunavyo weza fikiri, maana hakuna watu hatari kama wafu
waishio na hakuna watu hatari zaidi kwa maadui zetu wa fikra kama wanajamii wenye uwezo mkubwa wa kufikiri. Kwa
kweli tumechelewa sana kimaendeleo ukilinganisha na tuliokuwa nao sawa miaka 50
iliyopita ndugu zetu Wachina na Korea. Hatuwezi fika huko bila kuanzia tengeza mbinu
za kufikiri kwa kina sasa. Kumbuka mteja wa mambo yaliyotokana na fikra pevu za
wengine(ambazo si zetu wa Tanzania/Afrika) ni sisi, na kamwe wanaotupatia mambo
haya hawatoruhusu sisi(Wateja) kufunguka kamwe. Hebu sasa tufunguke.

Comments
Post a Comment