JE? TUNATUMIA VILIVYO UMOJA WETU WA KIIMANI KULETA MAENDELEO YA KIDUNIA KAMA WAAFRIKA



Ni nia ya dhati inayowafanya watu katika jamii husika kufikia malengo yao na ni mipango madhubuti inayofanikisha malengo hayo, lakini kama mipango haina uhai ndani yake sidhani kama malengo yatafikiwa. Kama watu weusi wanaoishi marekani( kaka , dada, mama na baba zetu) wanaweza kutoa sadaka ya dola za kimarekani millioni 252 (takwimu zilizokusanya na watafiti huru)  kwa kila jumapili sawa na zaidi ya billioni 568 za kitanzania na ili hali hawana hata mabenki yao, shule zao wenyewe, hospitali, taasisi za kifedha , mifumo ya usambaji na viwanda hali kadhalika na uwekezaji madhubuti. Hebu fikiria jumla ya billioni 14 za kimarekani ambazo ni ma trillioni ya kitanzania yanatumika kama sadaka na fungu la kumi, wakati wanategemea huruma ya weupe kupata mahitaji yao ikiwa ni zaidi ya asilimia 40 ya watu weusi. Kuna haja ya kuwa na kanisa lenye utajiri wa mabilioni wakati waumini wake hawawezi hata jihudumia kikamilifu? Je Malengo ya millenia yatafikiwa kweli?

Pesa inayochumwa na mtu si haki yangu kuiongelea ila kama hata senti moja ya mtu/watu fulani inatumika katika mfumo usio na manufaa na senti hiyo itaweza okoa nafsi za wengi, nina amini kuna haja ya kuisemea. Sina kipingamizi na hili suala la kumtolea Bwana ila je ? Tunatumia rasilimali zetu tulizonazo kwa umakini maana kama tunaweza toa pesa nyingi hivi( nikimaanisha waafrika walioko nje ambao ni sawa na sisi ukiwa na mrengo wa afrika moja) kwa ajili ya kuabudu tu na si kingine ,hakuna haja ya kulaumu juu ya maswahibu ya kiuchumi yanayotukabili, ikiwemo kuachwa kiuchumi , kiteknolojia na katika nyanja lukuki na wenzetu wachina pamoja na wazungu waliotutawala na wanaoendelea kututawala bila pingu wa kengele.

Hii inadhihirika hata kwetu huku (Kusini mwa jangwa la Sahara), naamini tuna uwezo mkubwa wa kufanya mengi zaidi tukifungua macho na kuona namna rasilimali zetu zinavyoweza kufanya kazi zaidi ya vile tunavyoweza fikiri. Takwimu zilizofanya na Pew survey (2010) ilionyesha kuwa asilimia 61.4 ya watanzania kuwa ni waumini wa dini ya kikristo, na asilimia zilizobaki kugawanyika kwa imani zingine, kwa namba zinavyo onyesha idadi kubwa ya watu ni wakristo ambao mafunzo ya dini yana wasihi kuwa watoaji wazuri, je? hatuwezi geuza mshale huu na kuangazia duru za kimaendeleo?

Hebu tuangalie pesa zinazotolewa katika sherehe mbalimbali, hafla zisizo na msingi katika jamii zetu, zingeweza fanya mambo mengi sana katika jamii kama mtu mmoja mmoja angejikita japo kwa nafasi aliyonayo kuwa katika wimbi linalo chegeza na kuleta mabadiliko, katika afya, usambazi wa huduma nyeti kwa jamii, elimu kwa watoto na watu wazima, kuwasaidia wasiojiweza, ulinzi wa raia na mali zao na ushirikiano wa pamoja.

Si vibaya kuabudu, sina hila na imani yeyote ile ( unaweza abudu chochote ) ila utaifa kwanza, tofauti zetu za kiimani, kikabila na kiitikadi zikae pembeni pale masuala ya taifa yanapohitaji umakini wetu  wa kuyanyambua hoja tata kwa weledi.

Bado sisi pamoja na ndugu zetu walioko Marekani tuko kwenye lindi la umasikini, ili hali tuna mtolea Mungu sadaka na zaka nyingi kushinda weupe (waliotutawala na waliotuletea hizi dini tunazozo shabikia kila leo) ambao wanazidi kuchochea upofu wetu katika mambo ya msingi. Tuna wachungaji matajiri sana kibao, wakati wajasiria mali waliowekeza kwenye kiini cha uchumi wachache sana, japo wapo wengi wanajitahidi kujitanua katika uwekezaji nawapongeza. Lakini bado hatuwezi lilia demokrasia, uhuru wa kuongea( kama vile haupo ) na propaganda zingine wakati bado mambo nyeti kama haya hatuyatilii maanani kabisa. Ni Afrika  na ni waafrika pekee ambao wanaweza kuabudu siku nzima hata kila siku ndani ya wiki, bila kupata maarifa/ujuzi wowote wa kutumia baada ya ibada katika dunia halisi ya ubepari. Kwa kweli sijawahi ona wala sikia mahubiri ambayo yanawa sihi waafrika kusimama imara na kuushinda ubepari wa mtu mweupe kwa kutumia mbinu za kidunia zenye msingi wa kiimani.

Miaka inakwenda na bado tunashikilia taratibu zile zile katika kuabudu ambazo bado hazitupeleki katika hatua za juu katika nyanja za maendeleo, laiti kama makanisa yetu yangekuwa yanatumika kama chombo cha kuwa andaa vijana kikamilifu kuivaa dunia hii isiyokuwa huruma kwa wanyonge na wasiokuwa na maarifa naamini lindi la umasikini lingekuwa chini. Kama tunaweza fanya harambee za kujenga makanisa makubwa (mahekalu) yenye vito vya thamani, iweje tushindwe (kwa kanisa moja moja) wasomesha vijana wetu wenye vipawa mbali mbali katika vyuo ili kupata maarifa na kuisaidia jamii/taifa kupanua kanisa zaidi. Kuacha Jesuit Fathers wanaofanya kazi nzuri, naona bado taasisi zingine za kidini zina nafasi kubwa sana ya kuangazia fursa mbali mbali zaidi ya ibada, nina jua kuna baadhi ya taasisi zimejikita hasa katika kutoa huduma za kielimu na afya (pongezi kwao kwa kazi nzuri), lakini vipi kuhusu zingine kama tafiti na uwekezaji katika teknolojia na huduma zinazo ijenga jamii na kulinda mazingira.

Nimeona jinsi imani inavyo tuunganisha sote na kuwa kitu kimoja. Ina ufanya tuwe ndugu na kuhuisha nafsi zetu kwa njia ya kipekee, inatufanya kuwa binadamu bora na kukwepa maovu. Licha ya hayo yote, kama kila siku ya ibada watu watatoka wakiwa na mistari mipya ya neno la Mungu na wakiwa na imani ya kuina paradiso naona tutakuwa bado hatuitendea kazi rasilimali tuliyonayo ambayo ni umoja wa waumini. Hakuna jambo gumu kama kuwaweka watu pamoja sehemu moja na kuwapa maarifa, naamini kabisa makanisa yetu yanaweza fanya zaidi ya kutoa mapepo na kutabiria watu utajiri. Maana dunia inabadilika kila siku, maarifa yanazidi potea na kupotoshwa na wale wasiotaka ona watu wakifunguka kifikra, hivyo basi kila rasilimali (watu, makanisa, maarifa ya waumini/viongozi, michango/sadaka) iliyopo mbele yetu inatakiwa tumika kusaidia sukuma gurudumu la maendeleo mbele kwa maendeleo ya taifa kwa ujumla na si imani husika, kwa kweli naona makanisa yetu bado hayajafanya kazi kubwa sana kulifanya hili kuwa uhalisia.

Uwepo wa imani ni mhimili wa maadili katika jamii maana bila hiyo, tutajionea mambo maovu sana. Viongozi wa imani wanajukumu kubwa la kuangazia nia ya imani zetu hizi. Kama hazitufanyi kwa namna moja au nyingine tuwe mabingwa wa uchumi, elimu na nyanja zingine naona kuna haja ya kuziangazia upya

Comments